Sunday 8 June 2014

Muigizaji Mkongwe Said Ngamba (Mzee Small) Afariki Dunia

 
Inna lillahi wa inna ilayhi raji'un
Sisi ni wa Allah nasi Kwake tutarejea.

Muigizaji mkongwe hapa nchini, Said Ngamba maarufu kwa jina la Mzee Small amefariki dunia usiku wa leo katika hospitali ya Taifa Muhimbili alikokuwa amelazwa akipatiwa matibabu ya Moyo baada ya kuugua kwa muda mrefu kabla ya kuzidiwa jana na kupelekwa Muhimbili.

Kwa muda mrefu Mzee Small alikuwa mgonjwa wa shinikizo la damu na aliwahi kueleza kuwa aligundulika kuwa na tatizo la damu kuganda kichwani lakini pia ugonjwa uliompelekea kulemaa mkono.

Akithibitisha taarifa ya kifo cha Mzee Small, mwanawe aitwae Mahmoud amesema mzee wake amefikwa na mauti hayo majira ya saa nne usiku wa tarehe 07.06.2014 kuamkia tarehe 08.06.2014 wakati akiwa hospitalini hapo akiendelea kupatiwa matibabu.

Mipango inafanyika nyumbani kwake Tabata.

Historia Yake Kwa Ufupi:

Said Ngamba au Mzee Small, alizaliwa mwaka 1955 na kupata elimu yake ya msingi katika shule ya Mingumbi huko Kilwa mkoani Pwani. Mbali na kuwa mkongwe, Mzee Small ndiye msanii wa kwanza kabisa Tanzania Bara kuchekesha katika luninga.

Mzee Small aliwahi kushiriki sanaa katika vikundi mbalimbali vya maigizo ya sanaa katika vikundi vya mashirika kama vile Reli, NASACO na mengine mengi, ambayo kwa sasa hayajihusishi tena na shughuli hizo.

Mzee Small huenda akawa anaaminika zaidi kuwa mmoja wa wasanii wakongwe nchini Tanzania, hasa katika fani ya uchekeshaji ambayo sasa inachezwa zaidi na vijana.

Allah ampokee mja wake, alijaalie kaburi lake kua ni Bustani katika mabustani ya Peponi.

Aamiyn

No comments:

Post a Comment